Friday, November 28, 2008

WEEKEND NJEMA

Mwaka 2008 upo mbioni kuelekea ukingoni mwake.Zimebaki wiki kadhaa tu kabla hatujaona zile fataki hewani na kusikia ving’ora vikitusindikiza kuumalizia mwaka.Kwa vyovyote vile mwaka 2008 utaenda na historia kadhaa zenyewe kuvutia kwa wengine na kutia simanzi kwa wengine.Ndio maisha.Ni mwaka ambao hakuna atakayeweza kamwe kusahau kwamba mtu mweusi wa kwanza amechaguliwa kuliongoza taifa kubwa la Marekani.

Lakini nchini kwetu pia ni mwaka ambao tunaweza kusema tumeshuhudia mengi ambayo siku za nyuma yalionekana kuwa hayawezekani.Tumeona viongozi kadhaa wakijiuzulu nyadhifa zao.Tumeshuhudia wengine wakipandishwa kwenye karandiga.Tumeona wazee wengine wakipandwa na pressure kwa sababu wanajua walishaharibu na hawana uhakika na kesho.Nadhani tunakubaliana kabisa kwamba miaka kadhaa ya nyuma,ilikuwa ni kama ndoto kusikia kiongozi akitangaza kujiuzulu.Mifano ya waliowahi kujiuzulu ilikuwa ni michache sana.

Inawezekana ni “changa la macho” na kwamba kinachofanyika ni mchezo wa aina yake wenye wingu zito la kisiasa.Inawezekana kabisa(hakuna lisilowezekana katika dunia hii).Lakini pamoja na yote hayo,tofauti na siku za nyuma,hata kile kitendo tu cha kuwaona waheshimiwa wakitokwa na jasho kwa sababu hawamo ndani ya yale “mashangingi” yao na badala yake wamekalia yale yale mabenchi ambayo hawakuwahi kuona umuhimu wa kuyakarabati kwa sababu “hayakuwahusu” na huku wakiwa wameegemea zile kuta ambazo hela yake ya rangi waliipeleka kusipotakiwa,ni vitu ambavyo vinaufanya mwaka 2008 uwe na lake katika historia.Bado tunasubiri kuona jinsi “changa la macho” litakavyopelekwa.Tupo na tunatizama kwa makini.Anayedhani tumelala anajidanganya.

Weekend njema!!

source-www.bongocelebity.com

No comments: